WAKULIMA TABORA WAOMBA AHADI ZA COP30 ZITEKELEZWE.


 

Na Hadija Omary Mazezele

Baadhi ya wakulima wa kata ya Ndevelwa, Manispaa ya Tabora, wamezitaka mamlaka husika na wadau wa maendeleo kuhakikisha ahadi zilizotolewa katika Mkutano wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi (COP30) zitekelezwe kwa vitendo ili kuwanufaisha wakulima, hususani katika miradi ya mabwawa ya maji, upatikanaji wa pembejeo na nyenzo za kisasa za kilimo.

Wakulima hao wamesema kuwa licha ya kuwepo kwa ahadi nyingi zinazolenga kuwasaidia wakulima kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, utekelezaji wake bado haujaonekana kikamilifu katika ngazi ya jamii.

Miongoni mwa wakulima waliotoa maoni yao ni Halima Musa, Juma Magodi na Hamisi Raulence, wakulima wa kata ya Ndevelwa, ambao wamesema kuwa utekelezaji wa ahadi za COP30 ni muhimu kwa ustawi wa kilimo na maisha ya wakulima wadogo.

Halima Musa alisema kuwa mabadiliko ya tabianchi yameendelea kuathiri uzalishaji wa kilimo, huku wakulima wakikosa miundombinu ya uhakika ya maji kama mabwawa ya kuvunia maji ya mvua, jambo linalofanya kilimo kutegemea mvua zisizotabirika.

“Ahadi zinazotolewa kwenye mikutano ya kimataifa kama COP30 zinapaswa kushuka hadi ngazi ya mkulima. Tunahitaji kuona mabwawa yanajengwa na miradi ya maji ikitekelezwa ili tuweze kulima kwa uhakika,” alisema Halima.

Kwa upande wake, Juma Magodi alisema kuwa upatikanaji wa pembejeo bora na kwa wakati ni changamoto kubwa kwa wakulima wa Ndevelwa, huku akisisitiza kuwa ahadi za kusaidia wakulima wadogo zinapaswa kutafsiriwa kwa vitendo.

“Tunaposikia kuna fedha na mipango ya kusaidia wakulima kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, tunatarajia kuona pembejeo, mbegu bora na nyenzo za kilimo zikifikishwa kwa wakulima, si kubaki kwenye makaratasi,” alisema Juma.

Naye Hamisi Raulence alisema kuwa uwajibikaji katika utekelezaji wa ahadi za COP30 ni jambo la msingi, akibainisha kuwa bila ufuatiliaji na utekelezaji thabiti, wakulima wataendelea kuwa waathirika wakuu wa mabadiliko ya tabianchi.

Wakulima hao wamezitaka serikali, wadau wa maendeleo na taasisi zinazohusika na masuala ya mabadiliko ya tabianchi kuhakikisha kuwa ahadi zinazotolewa katika mikutano ya kimataifa kama COP30 zinapangwa, kufuatiliwa na kutekelezwa kwa uwazi ili kuleta mabadiliko halisi katika maisha ya wakulima.

 

Post a Comment

0 Comments