Na Hadija Omary Mazezele
Wakulima mkoani Tabora
wameonesha uelewa mzuri kuhusu maana na umuhimu wa Mkutano wa Kimataifa wa
Mabadiliko ya Tabianchi COP30, wakisema kuwa uelewa huo utawasaidia kufuatilia
kwa karibu mikutano ijayo ya COP ili kunufaika na huduma za hali ya hewa pamoja
na ajenda zitakazojadiliwa.
Miongoni
mwa wakulima waliopata uelewa huo ni Kidumila Mtandi, Asha Salumu na Joseph
Wilson, wakulima kutoka kijiji cha Chang’ombe, wilaya ya Tabora ambao
walifuatilia mkutano wa COP30 na kuelewa kwa kina masuala yaliyojadiliwa.
Wakulima
hao walisema kuwa kupitia ufuatiliaji wa COP30, wamepata ufahamu kuhusu namna
dunia inavyojadili mabadiliko ya tabianchi, athari zake kwa kilimo, pamoja na
hatua zinazochukuliwa kuboresha upatikanaji wa huduma za hali ya hewa kwa
wakulima wadogo.
“Nimeelewa
kuwa mikutano ya COP inajadili mambo yanayotugusa moja kwa moja kama wakulima,
ikiwemo taarifa za hali ya hewa, mbinu za kukabiliana na ukame na mvua
zisizotabirika,” alisema Kidumila Mtandi.
Kwa
upande wake, Asha Salumu alisema kuwa uelewa wa COP30 umemsaidia kujua umuhimu
wa kufuatilia mikutano ijayo ili kupata taarifa zitakazosaidia kupanga shughuli
za kilimo kulingana na mabadiliko ya hali ya hewa.
Naye
Joseph Wilson alisema kuwa maarifa waliyoyapata yatawasaidia kuelewa vyema kile
kinachozungumzwa katika mikutano ijayo ya COP, hususan masuala yanayohusu
huduma za hali ya hewa, teknolojia rafiki kwa mazingira na fursa za kuwawezesha
wakulima kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Wakulima
hao wamesema kuwa kufuatilia mijadala ya COP kutawasaidia kuongeza uzalishaji,
kupunguza hasara zitokanazo na mabadiliko ya tabianchi, na kushiriki kikamilifu
katika jitihada za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi katika
jamii zao.

0 Comments